Wednesday, August 5, 2009

HALMASHAURI WILAYA YA KYELA YASHINDWA KUTUMIA SH.MILIONI 700

MKURUGENZI wa halmashauri ya wilaya Kyela, Harold Senyagwa, amefanya ukaguzi wa ghafla na kubaini jumla ya shilingi 738,317,808 zilizokuwa zimetengwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2008/09, hazijatumika.

Kufuatia hatua hiyo, ameunda Timu ya Ukaguzi ya watu watatu ili kufanya uchunguzi zaidi kujua sababu zilizopelekea kiasi hicho cha fedha kukaa bila kutumika hadi mwaka mwingine wa fedha unaanza.

Akithibitisha hilo kwa mwandishi wa habari hizi jana ofisini kwake, Senyagwa alisema kuwa alifanya ukaguzi huo Juni 15,mwaka huu wakati zimebakia siku kumi na tano kabla ya mwaka wa fedha kumalizika ili kujua kiasi cha fedha kilichotumika.

Mkurugenzi huyo Mtendaji alizitaja baadhi ya idara zilizobakiza fedha na kuwa ni Afya kwa upande wa ‘Busket fund’ sh.milioni 40.4, Mpango wa Maendeleo ya Afya ya Msingi (MMAM) sh.milioni 45.4, Ukimwi sh.140.8 na Kilimo na Mifugo sh.milioni 400.

“Lakini tumebaini pia kuna fedha nyingine ziliingia Juni 12,mwaka huu ambazo ni za MMAM sh.24.4 na RWSSP shilingi milioni 41.2.Hivyo ilikuwa ni vigumu kwa fedha hizo kutumika bila kufuata utaratibu uliowekwa na serikali” alisema Senyagwa.

Aliongeza kuwa aliwaandikia barua wakuu wa Idara ambao hawakutumia fedha zao walizokuwa wametengewa ambapo baadhi aliridhika na maelezo waliyoyatoa na wengine hakuridhika na maelezo yao.

Alizitaja idara alizoridhika na maelezo waliyotoa kuwa ni za MMAM, RWSSP na Kilimo ambao nao walipata fedha nyingine kiasi cha shilingi milioni 70 mwezi Machi, mwaka huu kwa ajili ya kuendeleza Kilimo.

Senyagwa alisema mbali ya kuunda timu ya kuchunguza sababu iliyopelekea fedha hizo zisitumike pia tayari ametoa taarifa hiyo kwa Kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango ya halmashauri hiyo juu ya suala hilo.

“Baada ya timu hii ya watu watatu kumaliza kufanya uchunguzi wao na kuniletea walichobaini itajulikana ni hatua zipi zichukuliwe” alisema Senyagwa.

Aliongeza kuwa pia hiyo ya Kamati ya Fedha imependekeza kuwa fedha hizo zaidi ya shilingi milioni 700 zifanyiwe Mpango mkakati wa kuhakikisha zinatumika ili zisiingiliane na bajeti ya mwaka huu wa fedha 2009/10.

Mkurugenzi alisema hivi sasa utekelezaji wake unaendelea lakini amewataka Wakuu wa idara ndani ya halmashauri ya Kyela, kuanza kuoredhesha na kukamilisha mahitaji mapema yakiwemo mambo ya tenda (zabuni).Senyagwa alisema:

”Kwa kufanya hivi itapelekea tusiwe na mambo kama haya ya kubakisha fedha hadi mwaka wa fedha unakwisha kwa miaka ijayo…lakini ikumbukwe kuwa mimi Mkurugenzi ndiye niliyeibua na kubaini kiasi hiki cha fedha kubaki”.

No comments:

Post a Comment