Wednesday, August 5, 2009

UVCCM YATOA UFAFANUZI KUHUSU RIDHWANI KIKWETE

UONGOZI wa jumuia ya Umoja wa Vijana ya Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), wilaya ya Kyela, umepinga uzushi unaonezwa kuwa Mjumbe wa Kamati ya Utekelezaji UVCCM Taifa, Ridhwan Kikwete, alizuiwa kushiriki harambee wilayani humo.

Imeelezwa kuwa UVCCM wilaya hiyo walimuomba Kikwete kuwa mgeni rasmi katika harambee hiyo iliyofanyika Julai 31,mwaka huu kwa kuwa ni kiongozi wa kitaifa wa jumuia hiyo na si vinginevyo.

Katibu wa UVCCM wilaya ya Kyela, George Silindu, aliyasema hayo wilayani humo kufuatia habari moja iliyoandikwa na gazeti moja la kila siku (jina linahifadhiwa) kuwa Kikwete aliingia mitini baada ya kuzuiwa na kundi moja la kisiasa wilayani humo.

Silindu alisema walianza kufanya mawasiliano na Kikwete kwa njia yam domo tangu mwaka 2008, ambapo mawasiliano rasmi ikiwa ni kumuandikia barua kupitia Katibu Mkuu wa UVCCM Taifa yalianza mwezi Februali mwaka huu.

“Tulimualika awe mgeni rasmi katika harambee yetu kwa ajili ya kutafuta mtaji wa UVCCM wilaya ya Kyela…Makadirio yetu yalikuwa ni kupata shilingi milioni 155 kwa awamu mbili tofauti” alisema Silindu.

Aliongeza kuwa Julai 31, mwaka huu baada ya kufanya mawasiliano na Mjumbe huyo wa Kamati ya Utekelezaji UVCCM Taifa, waliandaa mapokezi eneo la Busale, ambapo walikaa hadi saa 11:00 jioni bila ya kiongozi huyo kutokea.

Alifafanua kuwa waliamua kurudi ukumbi wa KBC uliopo Kyela mjini, ambako ndiko harambee ilikuwa ifanyike wakiwa wameongozana na viongozi wa UVCCM mkoa wa Mbeya pamoja na wawakilishi wa CCM mkoa ambao waliongozwa na Katibu wa Uchumi na fedha Keneth Ndingo.

Katibu huyo wa UVCCM wilaya alisema iliwabidi kuendesha harambee hiyo kama walivyokuwa wamepanga, lakini walishindwa kutangaza kiwango kilichopatikana kwa kuhofia kuwa Kikwete anaweza kutokea wakato wowote wakiwa ukumbini humo.

Silindu alisema Kamati maalumu ya harambee hiyo leo (jana), ilikuwa inatarajiwa kukutana kwa ajili ya kufanya tathmini nzima ya harambee hiyo na ndio itatangaza kiasi cha fedha kilichopatikana.

Aliongeza kuwa mbali ya kuendesha harambee hiyo, Kikwete pia alikuwa amepangiwa kazi ya kufungua matawi mawili ya UVCCM katika maeneo ya Ipinda na Ngyeke yaliyopo kata ya Matema na baadaye ahutubie mkutano wa hadhara katika kata hiyo.

“Tulimualika Kikwete kwa kuwa ni kiongozi wa kitaifa wa UVCCM,lakini hatukumualika kwa makusudi mengine yoyote kama inavyoenezwa…hivyo siyo sahihi kuwa alizuiwa kuja Kyela na kundi moja la kisiasa wilayani humu” alisema Silindu.

Alifafanua kuwa Kikwete asingekuwa kiongozi wa jumuia hiyo ngazi ya kitaifa, ndio ilipaswa watu wahoji kuwa ameenda wilayani humo kama nani lakini itambulike kuwa ni kiongozi wa kitaifa na ndiyo iliyoisukuma jumuia hiyo kumualika.

Silindu alisema kuwa UVCCM wilaya hiyo haiwezi kushtushwa na Kikwete kutohudhuria harambee, kwani naye ni binadamu kama walivyo wengine hivyo anaweza kupata udhuru uliopelekea ashindwe kufika wilayani Kyela.

Alibainisha kuwa wapo viongozi wengine waliowatumia kadi za mwaliko wakiwemo kutoka Dar es Salaam lakini walishindwa kufika, ila walituma michango yao waliyoahidi hivyo kutofika kwa Kikwete kusiwe nongwa.

“Kwa mtu mwenye shaka yoyote juu ysa ujio wa Kikwete ni vyema awasiliane na Mwenyekiti wa UVCCM wilayani hapa, Dk.Hunter Mwakifuna ama mimi ili tumpe ufafanuzi lakini siyo kuzusha mambo ambayo hayapo” alisema Silindu kwa msisitizo.

No comments:

Post a Comment