Wednesday, August 5, 2009

JAMBAZI LAUAWA NA WANANCHI KWA KUCHOMWA MOTO

MTU mmoja anayetuhumiwa kuwa jambazi, ameuawa kwa kupigwa na baadaye kuchomwa moto na wananchi wenye hasira kali wa mji mdogo wa Mlowo, wilayani Mbozi.

Tukio hilo lilitokea jana saa 11;00 alfajiri baada ya jambazi huyo akiwa na mwenzake mmoja aliyefanikiwa kukimbia, kukurupushwa eneo la darajani na sungusungu waliokuwa doria.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, wakazi wa mji huo walisema kuwa Sungusungu hao wakiwa doria waliwakuta watuhumiwa hao wawili wakiwa na nondo pamoja na mapanga, hali iliyoonyesha kuwa walikuwa wakienda kufanya uharifu.

Walisema mara baada ya kukurupushwa, mmoja alifanikiwa kukimbia na kumuacha mwenzake ambaye alipata kipigo kikali hadi kupoteza fahamu ambapo waliwaacha baadhi ya sungusungu wakimlinda na wengine kuendelea kumtafuta aliyekimbia.

“Mmoja wa watuhumiwa hao alifanikiwa kukimbia na ilidaiwa kuwa amejificha katika nyumba ya kulala wageni iitwayo Altimalta iliyopo Mlowo.Viongozi wa serikali ya mtaa walilazimika kuwaomba wananchi waliokuwa wamejitokeza kuondoka eneo hilo lakini ilishindikana” walisema.

Kufuatia hali hiyo baadhi ya raia wema walikimbilia kituo kidogo cha polisi Mlowo na kutoa taarifa ambapo walifika katika nyumba hiyo ya kulala wageni na kuwataka wananchi kuondoka lakini waliendelea kukaidi amri hali iliyowalazimisha polisi kutumia mabomu ya machozi kuwatanya.

Polisi walifanikiwa kuwakamata Paulo Dulle na mhudumu wa nyumba hiyo ya wageni,aitwaye Taida ambapo wananchi wakiwa mikono mitupu waliandamana hadi kituoni hapo na kuwataka polisi wamuachie Dulle ili wamuue pia.

Naye Meneja wa nyumba hiyo ya kulala wageni Altimalta, Furaha Mgalla alisema Julai 1,mwaka huu, aliwapokea wapangaji watatu aliowataja kuwa ni Ezekia Mbope, Paulo Dulle ambaye ni mpiga ramli, mkazi wa Tunduma na Salum.

Mgalla aliongeza kuwa jana saa 5:00 usiku, kulitokea ugomvi wa kimapenzi kati ya mhudumu wake aliyemtaja kwa jina moja la Taida na mpangaji Dulle, hali iliyopelekea aingilie kati ili kuleta suluhu.

“Baada ya kuwafuata mhudumu wangu Taida alidai kuwa Dulle alitaka kumkaba na amempora shilingi 80,000, ambapo nilipomuuliza Dulle hakutaka kuongea na badala yake alitoka nje.Mwenzake Salum alipoelezwa kilichojiri alianza kumpiga Dulle”alisema Mgalla.

Aliongeza kuwa kelele za ugomvi huo ziliwafikia Sungusungu, ambao walifika eneo hilo na kuwakamata Taida pamoja na Salum na kuwapeleka kituo kidogo cha polisi Mlowo, lakini Dulle alikataa kukamatwa.

Mgalla alisema ndipo Sungusungu hao walipotoka hapo na kuendelea na doria ambapo, waliwakuta vijana hao wawili eneo la darajani wakijianda kwenda kufanya uharifu na kuwazingira ambapo mmoja alifanikiwa kukimbia.

Taarifa zaidi zilizopatikana kwa watu walishuhudia tukio hilo, walisema mara baada ya kumuacha majeruhi huyo na kuanza kumfuata mwenzake aliyekuwa amekimbia, nyuma baadhi ya Sungusungu waliokuwa wameachwa na majeruhi huyo waliamua kutafuta majani na kuanza kumchoma moto mtuhumiwa.

Zilidai kuwa ndipo mtuhumiwa huyo alipokurupuka huku akipiga kelele, na kwenda kujitumbukiza katika mto ulio karibu na eneo hilo ili kuuzima moto uliokuwa ukiwaka mwilini mwake, na kelele hizo zilivuta kundi la watu waliofika na kumpiga na kisha kumchoma moto.

Imeelezwa kuwa Sungusungu hao walioondoka na kwenda moja kwa moja katika nyumba ya kulala wageni Altimalta kwani inadaiwa kuwa walikuwa na mashaka na kundi la watu hao watatu waliokuwa wamepanga hapo kuwa ni majambazi.

Hivyo walihisi kuwa mtuhumiwa aliyekimbia ni mmoja wa wapangaji watatu waliokuwa wakiwatilia mashaka, ambap walipofika waliizingira nyumba hiyo ya wageni ili kuhakikisha kuwa hakuna anayefanikiwa kutoroka.

Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Advocate Nyombi, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo la mauaji lakini alisema marehemu hajatambulika jina na kwamba wanawashikilia watu wawili kwa upelelezi zaidi.

Nyombi aliongeza kuwa mwili wa marehemu umehifadhiwa hospitali ya wilaya Vwawa.

No comments:

Post a Comment