Wednesday, August 5, 2009

WAGOMEA KULIPWA FIDIA KIDUCHU KUPISHA UJENZI WA SOKO JIPYA LA MWANJELWA

WAMILIKI 30 wa nyumba zinazotaka kubomolewa kata ya Ruanda, ili kupisha ujenzi wa soko jipya la kisasa la Mwanjelwa, wamepinga kiwango kidogo cha fidia wanachotaka kulipwa na halmashauri ya jiji la Mbeya.

Imeelezwa kuwa halmashauri hiyo imetenga kiasi cha shilingi Bilioni 1.1 kwa ajili ya kulipa fidia huku kiwango cha juu cha fidia kikiwa ni sh.milioni 82.3 na cha chini ni sh. milioni 9.

Soko la awali Mwanjelwa lililokuwa na wafanyabiashara zaidi ya 900, liliungua na kuteketea kwa moto Desemba mwaka 2006, na kupelekea hasara ya mamilioni ya shilingi.

Wamesema kuwa wanatarajia kuandika barua kwa Mkurugenzi wa jiji kupinga kiwango wanacjhotaka kulipwa na iwapo watapuuzwa basi watafungua kesi mahakamani kupinga nyumba zao kubomolewa.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, walisema kuwa nyumba zao hizo zimekaa kibiashara kwani zipo katika mtaa wa soko ambapo wenzao walio umbali wa mita 50 wamekuwa wakiziuza nyumba zao kati ya shilingi milioni 400 hadi milioni 200.

Vitus Swalo mwenye nyumba namba R/049 alisema kuwa yeye licha ya kumiliki nyumba kubwa ya kibiashara anashangaa kuwa katika uthamini uliofanywa na maofisa wa kitengo cha uthamini cha jiji kilichopo chini ya Edina Mwaigomole, anatakiwa kulipwa fidia y ash.milioni 11 kitu ambacho hawezi kukubaliana nacho.

Swalo alisema wao wanakubali nyumba zao kubomolewa ili kupisha ujenzi wa soko hilo lililotengewa jumla ya shilingi Bilioni 13 kwa ajili ya ujenzi wake, lakini hakubaliana na fidia anayotaka kulipwa kwani hailingani na eneo ilipo nyumba yake.

“Fedha ya fidia tunayotaka kulipwa na halmashauri ya jiji la Mbeya ni ndogo na mbaya zaidi ni kuwa hailingani na hasdhi ya jiji bali ni ile ya halmashauri…hatukatai kupisha ujenzi lakini kiwango hatukubaliani nacho” alisema Swalo.

Naye Keneth Mbewe mwenye nyumba namba R/.004 alisema wanapinga kiwango kidogo walichotengewa kwa ajili ya fidia na wanaiomba serikali kuingilia kati ili haki iweze kutendeka na wapate fidia ya kiwango kinacholingana na eneo hilo la kibiashara zilizopo nyumba zao.

Mbewe alisema kuwa wanataka kumuandikia barua Mkurugenzi wa halmashauri ya jiji la Mbeya, Elizabeth Munuo, kupinga kiwango hicho kidogo cha fidia na iwapo ombi lao halitasikilizwa basi wapo tayari kwenda Mahakamani kusimamisha zoezi hilo la ubomoaji wa nyumba zao.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa mtaa wa Soko, zilizopo nyumba hizo, Baraka Mwakyabula, alisema uthaminishaji wa nyumba hizo hauendani na hadhi ya jiji licha ya kwamba wananchi wake wameelezwa kuwa eneo hilo linatakiwa lijengwe soko la kisasa lenye hadhi ya jiji.

Naye Diwani wa kata ya Ruanda, Ephraim Mwaitenda, alipofuatwa alikiri kuwa baadhi ya wananchi wanaomiliki nyumba zinazotakiwa kubomolewa ili kupisha ujenzi wa soko hilo jipya, wamelalamikia kiwango kidogo cha fidia wanachotaka kulipwa.

Mwaitenda alisema lakini fedha hizo wanalipwa kulingana na uthamini uliofanywa na kitengo cha Uthamini cha halmashauri ya jiji la Mbeya, kulingana na matofali yaliyotumika kujenga nyumba husika.

“Baadhi ya nyumba zimejengwa kwa matofali ya saruji, matofali ya kuchoma na nyingine zimejengwa kwa matofali mabichi…kwa mantiki hiyo ni wazi kuwa wale waliojenga kwa matofali ya saruji (Block), watalipwa fidia kubwa zaidi” alisema Mwaitenda.

Aliongeza kuwa amewataka wamiliki hao waliokuwa wanapinga kiwango hicho cha fidia kurudi majumbani mwao, kuchukua karatasi za uhakiki na kisha kuzilinganisha na thamani halisi ya nyumba zao.

Mwaitenda alisema:”Nimewataka baada ya hapo iwapo wataona kuwa hawajaridhika na kiwango cha fidia wanachotaka kulipwa wauone uongozi wa jiji la Mbeya, ili suala lao lipatiwe ufumbuzi”.

No comments:

Post a Comment