Wednesday, July 29, 2009

WALIMU JIJINI MBEYA WAZUSHA TIMBWILI OFISI ZA JIJI NA BAADAYE KWA DC.

KUNDI la Walimu zaidi ya 100 wakiwa na jazba jana walivamia ofisi za Elimu na baadaye ofisi za Mkuu wa wilaya ya Mbeya, Leonidas Gama, wakilalamikia kucheleweshewa malipo yao bila chochote kulipwa tangu mwaka 2001 hadi 2007.

Kitendo hicho cha walimu kuzingira ofisi za elimu jijini hapa saa 2:00 asubuhi, kilipelekea baadhi ya watendaji kuzikimbia ofisi zao wakihofia kuwa wangeweza kupata kipigo kutoka kwa walimu hao.

Walidai kuwa wamekuwa wakifanywa wapumbavu na wanyonge ambapo wamekuwa wakitakiwa kuwasilisha kumbukumbu zao za madai ambapo mchakato umekuwa ukizidi kurefushwa.

Wakizungumza na waandishi wa habari waliofuatilia tukio hilo, walimu hao walisema kuwa waliambiwa waende ofisi hizo kati ya Julai 20 na 24 mwaka huu lakini kila mwalimu aliyefika hapo aliambiwa arudi siku nyingine huku wengine wakitakiwa kuwasilisha vielelezo vya madai yao wakati walikwisha kuviwasilisha awali.

Waandishi walifanikiwa kufika ofisi hizo za Ofisa Elimu wa jiji na kukutana na msongamano wa walimu hao waliokuwa wakidai hawawezi kuondoka ofisini hapo hadi madai yao yafanyiwe kazi.

Wakizungumza wakiwa katika makundi, walisema kuwa malimbikizo hayo ni mishahara, nauli za likizo,marekebisho ya mishahara yao kwa waliopandishwa vyeo huku waliorekebishiwa madaraja hawajawahi kupata mishahara mipya kwa muda wa miaka saba.

Naye Ofisa Elimu wa jiji la Mbeya, Aurelia Lwenza alipfuatwa alisema kuwa hajui lolote kuhusu mchakato mzima wa madai hayo ya walimu kwani mchakato mzima ulikuwa ukifanywa na idara ya utumishi kwa kushirikiana na Tume ya Utumishi wa Walimu(TSD), ofisi yake haikhusiki na madai hayo.

Aurelia aliongeza kuwa hana taarifa na uvamizi wa walimu hao isipokuwa walipofika alilazimika kumuita Ofisa Utumishi anayeshughulikia madai hayo awaondoe walimu hao kwani ofisi za TSD zipo.

Baadaye ndipo kundi hilo la walimu lilipovamia ofisi za Mkuu wa wilaya ya Mbeya, Gama ili kuwasilisha malalamiko yao, lakini hawakufanikiwa kumkuta kwani na kuelezwa kuwa yupo safarini jijini Dar es Salaam.

Kwa upande wake Ofisa Utumishi wa jiji, Lucy Timba hakuweza kuweka wazi kuhusu madai ya walimu hao na na kwamba haelewi sababu zilizowafanya wakusanyike kwenye ofisi hizo badala ya kuutumia muda huo kufundisha.

Lucy alithibitisha wito wa kuitwa kwa walimu hao uliotolewa na Katibu wa Tume ya Utumishi ya Walimu jiji la Mbeya,Fredy Lucas ambaye hakuweza kupatikana kwani yupo mkoani Morogoro kikazi.

No comments:

Post a Comment