Wednesday, July 29, 2009

WALIMU JIJINI MBEYA WAZUSHA TIMBWILI OFISI ZA JIJI NA BAADAYE KWA DC.

KUNDI la Walimu zaidi ya 100 wakiwa na jazba jana walivamia ofisi za Elimu na baadaye ofisi za Mkuu wa wilaya ya Mbeya, Leonidas Gama, wakilalamikia kucheleweshewa malipo yao bila chochote kulipwa tangu mwaka 2001 hadi 2007.

Kitendo hicho cha walimu kuzingira ofisi za elimu jijini hapa saa 2:00 asubuhi, kilipelekea baadhi ya watendaji kuzikimbia ofisi zao wakihofia kuwa wangeweza kupata kipigo kutoka kwa walimu hao.

Walidai kuwa wamekuwa wakifanywa wapumbavu na wanyonge ambapo wamekuwa wakitakiwa kuwasilisha kumbukumbu zao za madai ambapo mchakato umekuwa ukizidi kurefushwa.

Wakizungumza na waandishi wa habari waliofuatilia tukio hilo, walimu hao walisema kuwa waliambiwa waende ofisi hizo kati ya Julai 20 na 24 mwaka huu lakini kila mwalimu aliyefika hapo aliambiwa arudi siku nyingine huku wengine wakitakiwa kuwasilisha vielelezo vya madai yao wakati walikwisha kuviwasilisha awali.

Waandishi walifanikiwa kufika ofisi hizo za Ofisa Elimu wa jiji na kukutana na msongamano wa walimu hao waliokuwa wakidai hawawezi kuondoka ofisini hapo hadi madai yao yafanyiwe kazi.

Wakizungumza wakiwa katika makundi, walisema kuwa malimbikizo hayo ni mishahara, nauli za likizo,marekebisho ya mishahara yao kwa waliopandishwa vyeo huku waliorekebishiwa madaraja hawajawahi kupata mishahara mipya kwa muda wa miaka saba.

Naye Ofisa Elimu wa jiji la Mbeya, Aurelia Lwenza alipfuatwa alisema kuwa hajui lolote kuhusu mchakato mzima wa madai hayo ya walimu kwani mchakato mzima ulikuwa ukifanywa na idara ya utumishi kwa kushirikiana na Tume ya Utumishi wa Walimu(TSD), ofisi yake haikhusiki na madai hayo.

Aurelia aliongeza kuwa hana taarifa na uvamizi wa walimu hao isipokuwa walipofika alilazimika kumuita Ofisa Utumishi anayeshughulikia madai hayo awaondoe walimu hao kwani ofisi za TSD zipo.

Baadaye ndipo kundi hilo la walimu lilipovamia ofisi za Mkuu wa wilaya ya Mbeya, Gama ili kuwasilisha malalamiko yao, lakini hawakufanikiwa kumkuta kwani na kuelezwa kuwa yupo safarini jijini Dar es Salaam.

Kwa upande wake Ofisa Utumishi wa jiji, Lucy Timba hakuweza kuweka wazi kuhusu madai ya walimu hao na na kwamba haelewi sababu zilizowafanya wakusanyike kwenye ofisi hizo badala ya kuutumia muda huo kufundisha.

Lucy alithibitisha wito wa kuitwa kwa walimu hao uliotolewa na Katibu wa Tume ya Utumishi ya Walimu jiji la Mbeya,Fredy Lucas ambaye hakuweza kupatikana kwani yupo mkoani Morogoro kikazi.

HOSPITALI YA RUFAA MBEYA WATAKIWA KUTENDA HAKI KATIKA MALIPO YA SAA ZA ZIADA.

UONGOZI wa hospitali ya Rufaa Mbeya, umetakiwa kuwalipa wafanyakazi wake malipo ya saa za ziada kwa kufuata ngazi za mshahara (TGHS), na siyo utaratibu uliopo sasa.

Imeelezwa kuwa uongozi huo umekuwa ukiwaweka maofisa katika makundi mawili, lakini wote wamekuwa wakilipwa saa za ziada kwa kima cha chini cha mshahara, hali ambayo inakuwa haiwatendei haki.

Hayo yalisemwa jana na Mwenyekiti wa Chama Cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE), hospitalini hapo, Ismail Zambi, wakati wa hafla ya kuwapa zawadi wafanyakazi bora wa Sikukuu ya Wafanyakazi duniani(Mei Mosi), mwaka huu, iliyofanyika hospitalini hapo.

Mgeni rasmi katika tukio hilo, alikuwa Rais wa Shirikisho la Vyama Vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Ayuob Omary.

Wafanyakazi saba walipewa zawadi zao akiwemo mfanyakazi bora wa hospitali hiyo kwa mwaka huu ambaye ni muuguzi mkunga, Regina Sithole, aliyezawadiwa shilingi 300,000.

Zambi alisema utaratibu huo unaofanywa na hospitali ya Rufaa Mbeya siyo sahihi kwani umekuwa unawatambua maofisa wenye elimu ya digrii kitu ambacho siyo sahihi.

"Tumekuwa tunawekwa matabaka mawili tofauti wakati kazi ni zile zile...hivyo ingekuwa vyema wangeweka utaratibu wa kuangalia TGHS kwani Utumishi unatutambua kuwa ni maofisa wakati uongozi wa hospitali unamtambua ofisa kuwa ni yule mwenye digrii" alisema Zambi.

Aliongeza kuwa pia kuna mapungufu mengine yaliyopo hospitalini hapo ikiwemo kutowapandisha vyeo wafanyakazi kwa wakati kwa mujibu wa taratibu zilizopo.

Mwenyekiti huyo wa TUGHE alisema vile vile kumekuwepo na tatizo la kutorekebishwa mishahara kwa wakati kwa wanaopandishwa vyeo, kutolipwa mapunjo ya mishahara kwa wanaopandishwa vyeo na kurekebishiwa mishahara yao.

Zambi alisema:"Tunaupongeza uongozi wa hospitali kwa kudumisha utaratibu huu wa kutoa zawadi kwa watumishi hodari wakati wa sherehe za Mei Mosi kwa kila mwaka...".

Naye Rais wa TUCTA Omary alipongeza hatua hiyo ya kuwapatia zawadi watumishi bora, lakini pia alikumbushia kuhusu umuhimu wa kufanya vikao mahali pa kazi kwa kufuata utaratibu uliopo.

Omary alisema kuwa kwa kupitia vikao hivyo uongozi na wafanyakazi wanaweza kuvitumia kuweka wazi kasoro mbalimbali zinazokuwepo na hivyo kuweza kuzipatia ufumbuzi wake.

"Kwa kuwapa zawadi watumishi wenu bora mnakuwa mnawajengea motisha zaidi ya kuwajibika zaidi" alisema Omary.

Wafanyakazi wengine waliopata zawadi zao za shilingi 150, 0000 kila mmoja ni Dk.Henry Mwakayoka, ofisa wa maabara Hilary Mchuka, ofisa muuguzi kitengo cha wajawazito na Watoto Meta, Mwanjaa Kasigwa na ofisa muuguzi kitengo cha huduma ya afya ya akili, Daina Ifwani.

Pia wamo Muuguzi mkunga wa kitengo cha kuhudumia wanaoishi na virusi vya Ukimwi, Eddah Sanjala na Ally Mbasha kutoka upande wa masijala katika sehemu ya utawala.

Monday, July 27, 2009

SUMATRA KUDHITI DALADALA ZISIZTIKETI KWA ABIRIA JIJINI MBEYA.

MAMLAKA ya Udhibiti Wa Usafiri Nchi kavu na Majini (SUMATRA), kanda ya nyanda za juu kusini, imeazimia kupambana na tatizo sugu la wamiliki wa daladala jijini Mbeya la kutopenda kutoa tiketi kwa abiria.

Imeelezwa kuwa tatizo la utoaji wa tiketi kwa abiria wa daladala jijini Mbeya, limekuwa sugu hali inayopelekea abiria wengi wanaotumia usafiri huo kuona kama ni kawaida kwa wao kutopatiwa tiketi.

Akizungumza ofisini kwake, Ofisa Mfawidhi wa SUMATARA kanda, Amani Shamaje, alisema kuwa wamedhamiria kukomesha tabia hiyo ambayo imekuwa kero kwa abiria wengi.

Shamaje alisema kuwa tatizo hilo lilikuwepo pia kwa mabasi yafanyayo safari kwenda wilayani, lakini hivi sasa limekwisha baada ya SUMATRA kuingilia kati na kuanza kuyakamata mabasi hayo na kutoza faini ya shilingi 250,000 kwa kila basi lililokuwa halitoi tiketi kwa abiria.

"Hivi sasa mabasi mengi yafanyayo safari za kwenda wilayani yamekuwa yanatoa tiketi kwa abiria...tatizo tulilonalo sasa ni utoaji wa tiketi kwa daladala zifanyazo safari hapa jijini Mbeya" alisema Shamaje.

Aliongeza kuwa waliamua kwanza kutilia mkazo suala la uvaaji wa sare kwa madereva na makondakta wa daladala na pia kupiga marufuku usimamaji kwa sehemu zisizo kuwa na vituo ambapo wameweza kufanikiwa kwa kiwango kikubwa.

Ofisa Mfawidhi huyo wa SUMATRA kanda ya nyanda za juu kusini, alisema utoaji wa tiketi kwa abiria wa daladala jijini Mbeya, limekuwa ni tatizo linalowasumbua kwa muda mrefu na wameamua kujipanga ili kuhakikisha kuwa wanalimaliza.

Alisema kuanzia sasa daladala yoyote inayofanya safari zake jijini Mbeya, ambayo itakuwa haitoi tiketi kwa abiria itakuwa inatozwa faini ya shilingi 250,000 au kifungo cha kuanzia mwaka mmoja ama kisichopungua miwili au adhabu zote kwa mpigo.

Katika hatua nyingine, Shamaje alisema kuwa wanaandaa mkakati wa kuwadhibiti madereva wa daladala zinazotoka jijini Mbeya kwenda mji mdogo wa Mbalizi, ambazo zimekuwa hazifiki mwisho wa safari na badala yake kuishia eneo la Iyunga na hivyo kupelekea usumbufu kwa abiria.

Alisema kuwa watakutana na Mkuu wa kikosi cha Usalama barabarani mkoa wa Mbeya, Ezekiel Mgeni, ili kuangalia njia sahihi za kukomesha tabia hiyo ambayo hufanywa kuanzia saa 12:00 jioni ambayo imekuwa inapelekea abiria walazimike kupanda mabasi mawili tofauti ili kukamilisha safari

."Huu ni usumbufu kwa abiria kwani unakuta gari limeandikwa kuwa linakwenda Mbalizi, lakini likifika Iyunga abiria wanaambiwa kuwa hapo ndio mwisho wa safari...hii ni usumbufu kwani huwalazimu abiria kupanda daladala lingine ili kuwawezesha kukamilisha safari" alisema Shemaje.
KIJANA huyu muuza viatu, ambao ni maarufu zaidi kwa jina la Machinga, aliyepo jirani na benki ya Stanbic jijini Mbeya, akiendelea na kazi huku mgongoni akiwa amembeba mtoto mgongoni
WATEJA wa kampuni ya simu za mkononi ya Vodacom, wakiendelea zoezi la kusajili namba zao katika ofisi za kampuni hiyo zilizopo jijini Mbeya, kama walivyonaswa na kamera yetu jana.


MARY MWANJELWA AKITOA MSAADA WA SHATI ZA CCM

MJUMBE wa Baraza Kuu la UWT Taifa, Mary Mwanjelwa akimkabidhi Katibu wa UWT wilaya ya Mbeya mjini, Sarah Mgoli, msaada wa shati zenye nembo ya CCM kwa ajili ya wajumbe wa Baraza la UWT wilayani humo.

KIKUNDI cha Uhamasishaji cha CCM kutoka kata ya Maanga, jijini Mbeya, kikitoa burudani kwa wajumbe wa Baraza la UWT wilaya ya Mbeya mjini, katika kikao kilichohutubiwa na Mary Mwanjelwa

MJUMBE wa Baraza Kuu la UWT Taifa, Mary Mwanjelwa (kushoto), akitoa msaada wa kadi 100 za UWT kwa Katibu wa jumuia hiyo wilaya ya Mbeya vijijini, Mgeni Ottoh.



MWENYEKITI wa CCM wilaya ya Mbeya vijijini, William Simwali, akimshukuru Mjumbe wa Baraza Kuu la UWT Taifa, Mary Mwanjelwa, mara alipotembelea ofisi za Chama na kutoa msaada wa sh.50,000 kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa jengo hilo ambao bado unaendelea.




BASI la kampuni ya Mabruku lenye namba za usajili T.495 AAV aina ya Scania lifanyalo safari zake kutoka Mbeya kwenda wilayani Chunya, likiwa limepata ajali katika eneo la Charangwa nje kidogo ya Chunya hata hivyo hakuna mtu aliyejeruhiwa katika ajali hiyo.




Thursday, July 23, 2009

WANAWAKEW WATAKIWA KUJITOKEZA KUWANIA UONGOZI SERIKALI ZA MITAA

WANAWAKE mkoani Mbeya, wametakiwa kujitokeza kwa wingi kuwania nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi ujao wa serikali za mitaa, kupitia Chama Cha Mapinduzi, kwani uwezo wa kuongoza wanao.

Imeelezwa kuwa kitu kinachowakwamisha wanawake kushinda nafasi mbalimbali za uongozi katika chaguzi ni tabia ya kuonea wivu na kupigana majungu na kutosaidiana.

Wito huo umetolewa na Mjumbe wa Baraza Kuu la Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), Mary Mwanjelwa, katika ziara zake za kutembelea wilaya zote za mkoa wa Mbeya kuwashukuru wanawake kwa kumchagua katika nafasi hiyo na pia kuangalia uhai wa jumuia na CCM kwa jumla.

Mary alisema umefika wakati wanawake wanatakiwa kujiamini kuwa wanaweza na kwa kufanya hivyo ni wazi hawataweza kushindwa kushinda katika nafasi mbalimbali watakazoomba kuwania kupitia Chama Cha Mapinduzi.

"Tujenge mahusiano mazuri baina yetu sisi wanawake ili tuweze kuasonga mbele, kwa maslahi ya Chama Cha Mapinduzi...tupo katika nafasi hizi kwa nia ya kukitumikia Chama na siyo nje ya hapo" alisema Mwanjelwa.

Aliongeza kuwa itakuwa sifa kubwa kwa CCM na wanawake mkoani hapa, iwapo wanawake wengi watashinda kwa kishindo katika uchaguzi ujao wa serikali za Mitaa.

Alisema, jumuia ya UWT mkoani hapa imekuwa inalegalega kutokana na wanawake kuendekeza majungu na kutopendana kwa sababu zisizokuwa za msingi hali ambayo haikijengi Chama bali inakibomoa.

Mjumbe huyo wa Baraza la UWT TAifa, alisema umefika wakati wanawake mkoani hapa na Tanzania kwa jumla kuachana na wale wanaowaona kuwa wamekuwa wanawachonganisha na kuendeleza majungu ndani ya jumuia na CCM Kwa jumla ili kukifanya Chama kizidi kuimarika na kukubalika kwa wananchi wengi.

Naye Katibu wa UWT mkoa wa Mbeya, Mwanaidy Mbisha, alisema uhai wa Chama na jumuia zake utaonekana pale wanawake watakapokuwa wanalipia kadi zao kwa wakati, kuingiza wanachama wengi na pia kuhakikisha kuwa wanavaa sare za Chama katika shughuli zozote za Chama.

Mwanaidy alisema pia wanawatakiwa kuhakikisha wanafanya vikao vya mara kwa mara kwa mujibu wa Katiba na kunapokuwa na tofauti baina yao basi ni vyema watumie vikao halali vya Chama kumaliza tofauti zao kwa maslahi ya CCM.

"Hamfanyi vikao vya jumuia katika ngazi zenu za matawi na kata...lakini nafikiri tatizo kubwa malokuwa nalo ni kudhani kuwa hamna ajenda za kuitisha vikao hivyo.Lakini hata suala la kuhamasisha kulipia kadi nalo mnaweza kulifanya kuwa ajenda ya kikao chenu" alisema Mwanaidy.

Katika ziara hiyo Mary amekuwa akitoa msaada wa shati za CCM, kwa wajumbe wa Baraza la UWT wa wilaya na kadi mia moja za UWT ili kuziwezesha ofisi za UWT Katika wilaya husika ziweze kutunisha mfuko na kuingiza wanawachama wengi zaidi.

MARY MWANJELWA AJITOLEA KUSOMESHA WATOTO YATIMA WANANE MBEYA

MJUMBE wa Baraza Kuu la Umoja wa Wanawake (UWT), kutoka mkoa wa Mbeya, Mary Mwanjelwa, amejitolea kusomesha watoto yatima wa kike wanane waliofaulu mtihani wa darasa la saba, kutoka wilaya zote mkoani hapa, lakini hawana uwezo wa kusomeshwa sekondari.

Hivyo amezitaka kamati za Utekelezaji za UWT za wilaya hizo, kufanya mchakato bila ya upendeleo ili kuwapata watoto hao yatima ambao yeye atawajibika kuwalipia ada na mahitaji yote muhimu katika sekondari za kata.

"Jukumu la kuwalea watoto hawa yatima ni letu sisi wanawake wote...serikali na taifa kwa jumla wameonyesha kuwajali watoto hawa hivyo imefika kipindi na sisi tuone jukumu hili ni letu" alisema Mary.

Hayo aliyasema katika ziara yake ya kushukuru kwa kuchaguliwa katika nafasi hiyo na pia kuangalia uhai wa jumuia ya UWT na Chama Cha Mapinduzi kwa jumla.

Ameongozana na Katibu wa UWT mkoa wa Mbeya, Mwanaidy Mbisha na Mjumbe wa Kamati ya Utekelezaji UWT mkoani hapa, Florence Mwakanyamale.

Mary alisema mwanamke ndiye uhai wa jamii yoyote ile na ndio maana hata kwenye suala la uzazi wa Mpango iwapo mwanamke atakataa kushiriki ni wazi suala hilo halitawezekana.

Aliwataka wanawake mkoani Mbeya kuwajali na kuwathamini watioto yatima waliopo katika maeneo yao ili nao waweze kujiona siyo wanyonge kwa vile tu walipoteza wazazi wao wote wawili.Mjumbe huyo wa Baraza Kuu la UWT Taifa alisema:

"Hivyo nawaombeni mfanye mchakato wa bila upendeleo wowote ili niweze kupata mtoto yatima wa kike ambaye amefaulu mtihani lakini hana kabisa uwezo wa kusomeshwa sekondari".Aliongeza kuwa ukimgusa mtoto yatima ama mjane ni wazi unakuwa umemgusa Mwenyezi Mungu.

Mary alisema aliomba nafasi hiyo ili kuwatumikia wanawake wa mkoa wa Mbeya, katika kuwaletea maendeleo lakini hilo litafanikiwa iwapo nao watatoa ushirikiano wa dhati na kujenga umoja baina yao.

"Wanawake wa mkoa wa Mbeya na sisi umefika wakati tunatakiwa tuone wivu kwa wanawake wenzetu wa mikoa ya kaskazini ambao wanazidi kupiga hatua za kimaendeleo lakini sisi tunaendelea kupigana majungu na kutopendana" alisema Mary.

Sunday, July 19, 2009

MWANAMKE AJIUA KWA KUJIRUSHA KUTOKA GHOROFANI

MWANAMKE aliyekuwa ametoka kujifungua, Hellena Kambanga (29) amejiua baada ya kujirusha dirishani akiwa ghorofani ya tatu, hospitali ya Rufani Mbeya, kitengo cha Wazazi Meta, alikokuwa amelazwa.

Imeelezwa kuwa Hellena alijirusha kutoka wadi namba nne iliyopo ghorofani, saa 11:00 asubuhi, mara baada ya kumalizia dripu ya damu aliyokuwa ameongezewa mwilini baada kuishiwa wakati wa kujifungua.

Akithibitisha tukio hilo jana, mdogo wa marehemu ambaye ni mwanafunzi wa chuo cha IFM Dar es Salaam, akiwa mwaka wa pili aliyejitambulisha kwa jina la Shida Kambanga, alisema marehemu ameacha mtoto huyo ambaye ana umri wa wiki mbili sasa.

Shida alikuwa akitoa maelezo hayo kwa kushirikiana na mdogo wake alijitambulisha kuwa anaitwa Amina.

Shida alisema hiyo ilikuwa ni mimba ya pili, kwa dada yake huyo ambaye alikuwa anaishi eneo la Mbagala jijini Dar es Salaam na mumewe, na alikuwa amekuja mkoani Mbeya ambako ndipo alipozaliwa kusalimia ndugu na jamaa.

“Alikuwa anaumwa homa za mara kwa mara ambazo ni za kawaida kwa mwanamke mjamzito…siku za kujifungua zilipotimia alifanikiwa kujifungua salama kitengo cha Wazazi Meta, lakini alikuwa amepungukiwa damu mwilini” alisema Shida.

Aliongeza kuwa mara baada ya kuongezewa damu, marehemu Hellena alikuwa anaendelea vizuri na siku moja baada ya kumaliza dripu ya mwisho ya damu aliyokuwa amewekewa ndio aliamua kujirusha kutoka dirisha.

Kwa mujibu wa mdogo huyo wa marehemu, inaonyesha kuwa Hellena hakuwa na uangalizi wowote kutoka kwa wauguzi wa zamu siku hiyo hali iliyopelekea aweze kuamka muda huo wa alfajiri, kupanda dirishani na kujirusha hadi chini.

Alifafanua kuwa kutokana na utaratibu uliopo kitengo hicho cha Wazazi Meta, ndugu huwa hawaruhusiwi kulala na mgonjwa hivyo walipofika saa 12:00 asubuhi kumjulia hali ndipo walipopewa taarifa hizo.

Shida alisema:”Mara baada ya kujirusha kutoka juu ghorofani, dada alipata majeraha ya ndani kwa ndani mwilini na alikuwa akilalamika maumivu makali ya mgongo hali iliyopelekea ahamishiwe hospitali ya Rufani Mbeya kwa matibabu zaidi”.

Aliongeza kuwa Hellena alifariki dunia siku ya pili tangu afikishwe hospitalini hapo, na tayari amezikwa katika makaburi ya Mianzini yaliyopo eneo la Nzovwe jijini Mbeya, ambapo mtoto wake mchanga amechukuliwa na mama yao kwenda kulelewa Dar es Salaam.

Naye Mkurugenzi wa hospitali ya Rufani Mbeya, Dk. Eliuter Samky alipofuatwa ili kutoa ufafanuzi kuhusiana na tukio hilo, alisema hana taarifa zozote hivyo hawezi kuliongelea suala hilo.

“Mimi sina taarifa kuhusu kutokea kwa tukio hilo, hivyo siwezi kutoa maelezo yoyote…ningekuwa nimepewa taarifa ningesema, kifupi hakuna tukio kama hilo hospitalini hapa” alisema Dk.Samky.

RAS MKOA WA MBEYA AWATIMUA WAANDISHI WA HABARI

WAANDISHI wa habari kutoka vyombo mbalimbali, jana walishindwa kuhudhuria kikao cha Mkuu wa mkoa wa Mbeya,John Mwakipesile na Jaji Mkuu Agustino Ramadhan, baada ya Katibu Tawala wa mkoa (RAS), Beatha Swai kuwazuia mlangoni.

Tukio hilo lilitokea jana saa 3:00 asubuhi, mara baada ya waandishi wa habari kufika hapo kuitikia wito uliotolewa na Ofisa Uhusiano wa Mahakama Kuu (PRO), Nurdin Ndimbe kuhudhuria kikao hicho bila kukosa.

Waandishi hao zaidi ya saba, walifika ofisi hizo muda waliotakiwa na walipotaka kuingia katika kikao hicho, walikutana nja kikwazo hicho kutoka kwa RAS Beatha akishirikiana na Msaidizi wa Mkuu wa mkoa (DPS), ambaye jina lake halikuweza kujulikana.

Hatua hiyo ni tofauti na taarifa iliyotolewa na Afisa Uhusiano huyo wa Mahakama Kuu, Ndimbe ambaye aliwaeleza waandishi kuwa wanatakiwa kushiriki kikamilifu katika ziara ya Jaji kuanzia ofisi ya Mkuu wa Mkoa na kwingineko.

Vikwazo hivyo vilianzia kwa Msaidizi wa Mkuu wa Mkoa (DPS) ambaye aliwaeleza waandishi kuwa hakuwa na taarifa ya waandishi kutakiwa kuingia katika ofisi hizo na kuwataka watoke nje wakasubiri.

Hata hivyo juhudi za waandishi kujaribu kumuelekeza umuhimu wa wao kuhudhuria mazungumzo baina ya Mkuu wa Mkoa na Jaji Mkuu ziligonga mwamba baada ya Katibu Tawala, Beatha kusimama mlangoni na kuwazuia baadhi ya waandishi kwa kuwasukumia nje ya ofisi.

Baada ya kuwepo kwa kutoelewana baina ya waandishi, msaidizi wa mkuu wa mkoa na Katibu Tawala, Afisa habari wa mahakama, Ndimbe aliwaomba waandishi wasubiri nje huku naye akiwa haelewi kinachoendelea na sababu za waandishi kuzuiwa.

Baadhi ya waandishi walilalamikia kitendo cha Swai kwa madai kuwa yeye pamoja Msaidizi wa Mkuu wa Mkoa wamekuwa na tabia ya kuwazuia waandishi na wakati mwingine kudai hawaruhusu kumuona Mkuu wa Mkoa bila ya kuwa na miadi naye.

Lakini tukio hilo liliwasikitisha waandishi wengi kwani ni tofauti na ushirikiano mkubwa alionao Mwakipesile tangu ateuliwe kushika nafasi hiyo, kwani amekuwa akiwataka waandishi kumuona muda wowote wanapokuwa na jambo la dhalura.

“Hawa wanatushangaza, sisi kumuona Mkuu wa Mkoa lazima tuwe na miadi hata kama kuna jambo la dharura, lakini ofisi ya Mkuu wa Mkoa huwa inaita waandishi bila ya kuweka miadi, hii ni ajabu kabisa” alisema.

Jaji Ramadhani jana alikuwa Mkoani Mbeya kwa ziara ya siku moja ambapo aliwasili Mkoani Mbeya akitokea Mkoani Rukwa.

MAREHEMU JOSEPH HILL WA KUNDI LA CULTURE

MUZIKI wa Reggae umetokea kujipatia mashabiki na wapenzi wengi duniani kutokana na mashairi yake siku zote kugusa maisha halisi ya binadamu.

Kifupi unalenga ukweli halisiNa ndio maana leo hii unapomtaja mwanamuziki mahiri na mfalme wa Reggae, marehemu Robert Nesta Marley maarufu zaidi kwa jina la Bob Marley, hata mtoto mdogo wa miaka mitano hawezi kupata kigugumizi kukueleza kuwa anazipenda nyimbo zake.

Lakini pia kuna waimbaji wengine mahiri wa muziki huu ambao mara nyingi wanamuziki wake hupenda kuziachia nywele zao kichwani kuwa ndefu yaani kufuga Rasta, kama kitambulisho cha muziki huo.Hata hivyo kuna wanamuziki wengine wa muziki huu hawana Rasta.

Mmoja wa waimbaji hao ambao nao wamejipatia sifa na kuutangaza muziki huu wa Reggae na kupelekea kujipatia umaarufu duniani ni marehemu Joseph Hill, kiongozi wa kundi la Culture.

Hill alikuwa ni kiongozi wa kundi hilo la Culture lililokuwa linaundwa na wasanii wakongwe ambalo lilitokea kujipatia sifa kubwa nchini Jamaika na duniani kwa jumla.

Mnamo Agosti 19, mwaka 2006, wapenzi na mashabiki wa reggae walipatwa na mshituko mkubwa kufuatia kifo cha msanii huyu mahiri aliyekuwa na sauti ya kipekee iliyoweza kumtoa nyoka pangani.

Hill alikutwa na mauti mjini Berlin nchi Ujerumani, baada ya kuugua ghafla akiwa katikati ya ziara ya kimuziki barani Ulaya na kundi na kundi lake la Culture.

Kutokana na mchango wake mkubwa Hill alitunukiwa tuzo nyingi ikiwemo ile iliyojulikana kama ‘Jamaika Reggae Walk of Fame and a 2005 Independence Award’ aliyotunukiwa na Waziri Mkuu wa Jamaika.

Kifupi ni kuwa unapokuwa unawaongelea magwiji wa muziki wa Reggae waliowahi kutokea hapa duniani, basi ni wazi lazima utalitaja pia jina la Hill kuwa miongoni mwao na hilo halina ubishi.

Kundi la Culture lililoundwa mnamo mwaka 1976, na kujizolea umaarufu mkubwa huku likijulikana pia kama Mitume ya Afrika, lilikuwa linaundwa na wasanii wakali wakiwemo Joseph Hill, Albert Walker na Kenneth Dayes.

Hill alikuwa ni msanii pekee ndani ya kundi hilo aliyekuwa na uzoefu wa mambo ya Studio, baada ya kuwa amewahi kufanya kazi katika studio ya Coxone Dodd's akiwa mmoja wa waandaaji wa nyimbo za kundi lililoitwa Soul Defenders mwanzoni mwa miaka ya 1970.

Muda mfupi baada ya kuanzishwa kwa kundi la Culture, lilianza kufanya kazi na mtayarishaji wa muziki aitwaye Joe Gibbs akiwa na Injinia wake Errol Thompson. Wakiwa na Gibbs walifanikiwa kurekodi albamu mbili zilizojipatia umaarufu mkubwa.

Mara baada ya kutolewa kwa albamu hizi mbili ambazo zilikuwa na mtazamo mchanganyiko wa historia ya Jamaika, na mtazamo mpya wa mabadiliko ya hali ya hewa. Baada ya kupata mafaniko wakiwa na Gibbs, kundi hilo lilihama na kwenda kufanya kazi na mtayarishaji mwingine aliyejulikana kwa jina la Sonia Pottinger.

Culture pia walianza kufanya kazi na wanamuziki wengine mahiri waliopo kama Robbie Shakespeare, Sly Dunbar, Ansel Collins na Cedric Brooks.Kampuni ya kurekodi ya Virgin ilichukua albamu yao iliyowafanya (Culture) , wazidi kuwa maarufu na kupata mashabiki hadi nje ya Jamaika.

Mwaka 1982 waimbaji watatu wa kundi hilo waliojiondoa na kuanza maisha yao kivyao, ambapo Joseph Hill aliendelea kutumia jina la Culture lakini baadaye mwaka 1986 waliungana tena na kurekodi albamu mbili zilizojizolea umaarufu mkubwa za 'Culture in Culture' na 'Culture at Work'.

Baadaye mwaka 1993 Kenneth Dayes aliondoka katika kundi na kubadiliwa kwa muda na muimbaji kutoka kundi la Dub Mystic, ambaye.

Wakiwa na Dub Mystic, Culture walifikia mafaniko ya juu kimuziki baada ya kuachia albamu za 'One Stone' na ‘Trust Me' na live albamu iliyokwenda kwa jina la 'Cultural Livity'. Baada ya kundi hilo kudumu kwa muda wa miaka 27,Joseph Hill na wenzake hawakuonyesha dalili za kushuka kiwango chao kimuziki.

Kundi la Culture liliendelea kuwa imara likiwa na msimamo wa kudumisha ukweli kuhusu asili ya muziki wa Reggae lakini pia muda mwingine likiingiza milio na sauti mpya katika muziki wao.

Wanamuziki wa kundi la Culture wameonyesha njia kuwa ni moja ya kundi bora la muziki wa Reggae lililoweza kutawala kuanzia katika utunzi wa mashairi ya albamu albamu zao hadi katika kulitawala jukwaa.

TOENI TAARIFA NA KUORODHESHA VIUATILIFU CHAKAVU

MKAGUZI wa mazao ya kilimo kutoka Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Damian Gasana, amewataka wananchi wa mikoa ya kanda za juu kusini, kutoa taarifa na kuorodhesha viuatilifu chakavu.

Alisema viuatilifu hivyo ambavyo vina athari kwa binadamu na mazingira vitakusanywa na watalaamu maalumu.

Gasana alisema kipindi cha mwaka 1997/1998, Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), lilifanya tathimini na kubaini kuwepo kwa tani 1,000 za viuatilifu na tani nyingine 200 za madawa ya chakavu ya mifugo.Taka hizo zimeonekana katika maeneo yasiyopungua 325 nchini kote.

Hayo aliyasema jana wakati akizungumza na waandishi wa habari kuelezea mradi wa Africa Stockpiles ambao una mkakati wa kukusanya viuatilifu hivyo kwa mikoa ya kanda hii.

Gasana wananchi wote wanawajibika kutoa taarifa sahihi za uwepo wa viuatilifu chakavu kwa mabwana shamba na ofisi ya kilimo ya wilaya ambapo alisema kuwa wananchi hawatakiwi kushika wala kuhamisha viuatirifu na kwamba kazi hiyo itafanywa na wataalamu maalumu waliofundishwa.

Alisema kuwa shughuli ya kutoa taarifa kuhusu viuatilifuy chakavu ni hiyari na kwamba hakuna hatua zozote za kisheria zitakazochukuliwa kwa wananchi watakaotoa taarifa juu ya uwepo wa viuatilifu, “viuatilifu ni neon linalotumika badala ya neno la dawa za kilimo”.

Alivitaja baada ya viuatilifu chakavu kuwa ni vyote vilivyoisha muda wake, vilivyopigwa marufuku kutumika nchini kisheria, bidhaa za viuatirifu zilizopondeka na kuharibika pamoja na vyombo au vitu vilivyoathirika au kuchafuliwa na viatilifu hivyo.

Aidha, Gasana alisema kuwa hiyo nafasi pekee ya kuisafisha nchi kuondokana na sumu zilizolundikana ambapo alisema kuwa ni jukumu la kila mwananchi kushiriki kutoa taarifa ili viatilifu hivyo viondolewe katika makazi ya wananchi pamoja na kuondokana na vyanzo vya uharibifu wa mazingira.

WASICHANA WA NZOVWE JIJINI MBEYA WANAPENDA KUPIGWA 'MTUNGO'

WASICHANA wa eneo la Nzovwe, jijini Mbeya wametuhumiwa kushinda katika klabu za kuuza pombe za kienyeji, hasa nyakati za usiku na kufanya mapenzi na wanaume zaidi ya mmoja kwa siku kwa tamaa ya fedha.

Imedaiwa tabia ya wasichana hao, kupenda kuomba fedha kwa wanaume tofauti wanaokuwa wanakunywa pombe katika klabu hizo, hupelekea mwisho wa siku wakubali kufanya ngono zembe na mwanaume zaidi ya mmoja.

Hayo yalisemwa kwa nyakati tofauti na wakazi wa eneo hilo, katika mkutano wa hadhara ulioandaliwa na Vijana Mabalozi Watanzania wanaoishi na virusi vinavyosababisha Ukimwi (TAYOPA).

Mkoa wa Mbeya ni wa nne kutembelewa na TAYOPA ambao wapo kuutambulisha mradi wao uitwao 'Vijana Tuzinduke ili kujikinga na Ukimwi'.

Mikoa mingine iliyotembelwa ni Dar es Salaam, Lindi, Mtwara na baadaye wataelekea Ruvuma.
Mradi huo unafadhiriwa kwa pamoja na na shirika la Afya la Kimataifa (FHL) na kituo cha televisheni cha MTV cha nchini Marekani.

Wakizungumza wakazi hao wa Nzovwe walisema kuwa wasichana wa kike wa maeneo hayo, wamekuwa wanaendekeza sana kuombas fedha kwa wanaume katika klabu za pombe nyakati za usiku hali inayopelekea kuwepo kwa ngono zembe na wanaume wengi kwa siku.

Mkazi aliyejitambulisha kwa jina moja la Joyce alisema hali hiyo imefanya wasichana hao ambao bado ni wanafunzi wa shule za msingi, kupenda kufanya ngono na wanaume wengi mtindo ambao ni maarufu zaidi kwa jina la 'Mtungo'.

"Huku unaweza kumuona msichana ukadhani ni mdogo, kumbe anao uwezo wa kufanya mapenzi na zaidi ya mwanaume mmoja kwa siku...kimsingi hali inatisha kwani huwa wanafanya ngono zembe".Joyce alisema

Naye Mwenyekiti wa TAYOPA, John Solanya, alisema yeye alipimwa afya na kugundulika kuwa na maambukizi ya virusi vya Ukimwi tangu mwaka 1995, ambapo alijitangaza.

Solanya alisema kuwa anaishi na mke pamoja na mtoto mmoja ambao hawajaambukizwa Ukimwi, na kuwa tangu mwaka huu hajawahi kuumwa hadi kufikia hatua ya kulazwa hospitalini kwani amekuwa anazingatia ushauri anaopewa.

"Nina mke na mtoto ambao wao hana maambukizi ya Ukimwi... ninapotaka 'chakula cha usiku' kutoka kwa mke wangu huwa tunatumia kondomu" alisema Solanya.

Naye Fitina Mohamed, ambaye pia anaishi na virusi vya Ukimwi, alisema ni wengi wanayo maambukizi ya ugonjwa huo lakini huwezi kuwatambua kwa kuwaangalia kwa macho bali hadi wapime na kujitangaza.

Alihoji kuwa ni nani ambaye angeweza kuwatambua kuwa yeye ama mwenzake Solanya wanaishi na virusi vya Ukimwi iwapo wangeamua kukaa kimya mara baada ya kupima afya zao, na kuendelea kukubali kufanya ngono zembe.

Tukio hilo lilipambwa na burudani kutoka kwa wasanii Fareed Kubanda 'Fid Q. na mshindi wa Bongo Star Search, Jumanne Idd ambao waliweza kutoa burudani kabambe na kuwa kifutio kikubwa katika mkutano huo.

JAJI MKUU WA TANZANIA ALONGA KUHUSU WATUHUMIWA WA UFISADI.

JAJI Mkuu wa Tanzania, Agustino Ramadhan, amesema mahakama haiwatambui watu wanaotuhumiwa kwa ufisadi kuwa mafisadi hadi pale ushahidi dhidi yao utakapopelekwa na kutiwa hatiani.

Alisema ni vyema wananchi wote wenye ushahidi unaoweza kuwatia hatiani watuhumiwa hao waupeleke mahakamani ili kesi hizo ziweze kukamilishwa lakini siyo kuingilia uhuru wa mahakama kwa kuilazimisha kuwatia hatiani.

“Tuleteeni ushahidi ili tuweze kuufanya kazi lakini hadi sasa hawa sisi mahakama tunawatambua kuwa ni watuhumiwa lakini siyo mafisadi…tukiruhusu kuingiliwa ni wazi uhuru wa mahakama utakuwa unachezewa” alisema Jaji Mkuu Ramadhan.

Jaji Mkuu Ramadhan ambaye ni Mwenyekiti wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, aliyasema hayo wakati akizungumza na wajumbe wa Kamati ya Mahakama wa wilaya zote na wale wa mkoa wa Mbeya, katika ukumbi wa Dk.Ali Shein.

Alisema umma unatakiwa usiiigilie mahakama katika utendaji wake wa kazi na kutoa mfano kuwa hata Yesu (Nabii Issa), alipopelekwa kwa Pilato ili amtie hatiani, Pilato alinawa mikono baada ya kuona kuwa mtu huyo hana hatia hivyo hawezi kumuhukumu kwa kuwa tu wayahudi wanataka ahukumiwe.

“Mfano huu ni mojawapo ya hofu ya uhuru wa mahakama unavyoweza kuingiliwa…na ndiyo maana Pilato alinawa mikono kuonyesha kuwa mahakama imemuona hana hatia hivyo haiwezi kumuhukumu pasipo kuwa na ushahidi” alisema Ramadhan.

Aliongeza kuwa hisia ya uhuru wa mahakama siyo ndio itamfanya Jaji Mkuu ashindwe kukaa na Rais Jakaya Kikwete, Waziri ama mkuu wa mkoa kwa madai atashindwa kufanya kazi yake ipasavyo.

Alisema:”Jaji Mkuu hawezi kumuingilia na kumuambia Jaji yeyote kuhusu nini cha kufanya kwa kesi iliyopo mbele yake, kwani Jaji ndie mwenye jukumu la kuiendesha kesi hiyo hivyo huwezi kumshika na vivyo hivyo umma nao unatakiwa usiingilie uhuru wa mahakama”.

Aidha, Jaji Mkuu Ramadhan alisema amekuwa anapokea barua nyingi kutoka kwa wabunge na wakuu wa wilaya nchini zikimtaka awahamishe mahakimu kutoka maeneo yao kwa kutuhumiwa kutowajibika katika utendaji wao wa kazi huku wengine wakituhumiwa kwa vitendo vya kupokea rushwa.

Alisema dawa ya tatizo hilo ipo mikononi wa Mtume hizo za Mahakama ambazo kazi yake kubwa ni kuhakikisha kuwa mahakimu wanakuwa na nidhamu na wanafanya kazi zao kwa kufuata misingi ya sheria iliyopo na siyo nje ya hapo.

Aliongeza kuwa kumhamisha hakimu kutoka sehemu moja kwenda nyingine siyo suluhisho, bali kinachotakiwa ni Kamati hizo kukutana mara kwa mara ili kuyafanyia kazi malalamiko wanayokuwa nayo kuhusu mahakimu katika maeneo yao.

Jaji Mkuu alisema:”Juhudi za Tume ni kushughulikia pia maslahi ya watumishi wote wa mahakama…ukiacha nidhamu kwa majaji na mahakimu, lakini pia kuna madhambi mengi yanafanywa na makarani pamoja na wahudumu wa mahakama zetu”.

POLISI WATATU WATUPWA LUPANGO KYELA

POLISI watatu wilayani Kyela, wanashikiliwa kwa tuhuma za kuwa chanzo cha vurugu zilizotekea wilayani humo mara baada ya raia Lucas Mwaipopo,mkazi wa Mbugani kuuawa kwa kinachodaiwa ni kipigo kutoka kwa polisi.

Vurugu hizo zilipelekea wananchi zaidi ya 500 kuvamia na kupiga mawe kituo cha polisi, kuchoma moto mahakama ya Mwanzo ya Kyela mjini na pia kufanya uharibu wa mali katika ofisi ya Mkuu wa wilaya hiyo.

Polisi hao watatu wanaoshikiliwa ambao wote wana cheo cha Masajenti kutoka kitengo cha upelelezi wametajwa kuwa ni John mwenye namba D.4067, Joseph mwenye namba F.4849 na Mussa mwenye namba F.5753.

Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya, Advocate Nyombi alisema jana kuwa polisi hao watatu wanashikiliwa ili kuhojiwa kuweza kupata chanzo cha vurugu hizo zilizotokea wilayani humo na kupelekea polisi kutumia risasi za moto na mabomu ya machozi kuwadhibiti wananchi hao.

Alisema kuwa endapo polisi hao watatu wanaotuhumiwa kuwa chanzo cha kuzuka kwa vurugu hizo, wakibainika kuwa ni kweli watachukuliwa hatua kali za kisheria ili kuwa fundisho kwa wengine.

Nyombi alisema kuwa watu 96 walikamatwa kwa tuhuma za kuchochea vurugu hizo, ambapo walihojiwa na kumi na watano (15), kati yo wamefikishwa mahakamani jana kwa kosa la kufanya vurugu na kuvamia kituo cha polisi.

Aliwataja polisi wanane waliojeruhiwa kwa kupigwa mawe kuwa ni mkuu wa upelelezi wa wilaya ya Kyela Richard Mchomvu, E.9945 PC Julius, G. 54 PC Nyanda, E.7201 PC Timoth, E.1787 Koplo Robert, D.9713 Koplo Sarafini, E.3732 Koplo Travael, na E.8631 Sajent Mwita.

Aidha, magari mawili ya polisi yenye nmba za usajili PT.0798, PT. 0799 yote aina ya Lanlover yaliharibiwa kwa kupigwa mawe huku magari mengine ni T.646 AYL aina ya Landlover mali ya Daniel Mwambulukutu na T. 279 ARJ aina ya Toyota Hiace.

Kamanda Nyombi alisema kuwa katika watu waliojeruhiwa katika vurugu hizo yumo Ofisa Maeneleo ya Jamii wilaya ya Kyela, Nulusigwa Mwakigonja ambaye gari lake lenye namba za usajili T.573 AFA lilipoteza uelekeo na kugonga mti ambapo limeharibika vibaya.

Taarifa nyigine zilizopatikana kutoka hopitali ya Rufani Mbeya, zilidai kuwa majeruhi Jackob Antony (24), ambaye alipigwa risasi iliyoingia tumboni na kutokea kwenye kalio lake la upande wa kulia alikuwa anplekwa chumba cha upasuaji kwa ajili ya kuondolewa risasi.

Kufuatia vurugu hizo polisi juzi walilazimika kutangaza hali ya hatari na kuwataka wananchi kuwepo majumbani mwao ifikapo saa 1:30 usiku hali iliyopelekea mji huo wa mpakani na nchi jirani ya Malawi kupooza huku mitaa yote ikiwa haina watu.

Ni Mtizamo Tu ilishuhudia baadhi ya wateja waliokutwa katika baa ya Half London, iliyopo mjini humo wakipewa misukosuko kwa kukaidi kutii amri hiyo baada ya kukutwa wakiendelea kunywa vinywaji.

Hali hiyo ilipelekea wageni wengi waliochelewa kupta chakula cha jioni kulazimika kulala njaa kwani hakuna hotel ama baa yoyote iliyokuwa inafanya kazi kutokana na amri hiyo ya hatari.

Kituko kingine kilikuwa ni pale msichana aliyetajwa kwa jina la Jenny Chawe, ambaye alikuwa salon iitwayo Mariam iliyopo Kyela mjini akirembwa kujiandaa na sherehe ya kuagwa, naye kupotea kufuatia vurugu hizo hali iliyopelekea ndugu zake kuanza kuhaha kumtafuta mitaani.

Pia baadhi ya wanawake walikutwa barabarani wakiwa wanahaha kuwatafuta watoto wao baada ya kupotezana nao kufuatia vurugu hizo, lakini walifanikiwa kuwapata baadaye hali ilipotulia.

Friday, July 10, 2009

MKUU WA ST.AGGREY SEKONDARI ABAKA MWANAFUNZI

MKUU wa shule ya sekondari ya St.Aggrey, jijini Mbeya Henry David Chelula, amefikishwa mahakama ya mkoa wa Mbeya, akikabiriwa na kosa la kutaka kumbaka mwanafunzi wa kike wa kidato cha nne shuleni hapo.

Chelula alikamatwa na maofisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), mkoani hapa baada ya kuwekewa mtego.

Kesi hiyo ya jinai namba 135 ya mwaka huu ipo chini ya mwendesha mashtaka, Wakili wa serikali Keneth Sekwao na inasikilizwa na Hakimu mkazi Deborah Ndyekura.

Ilidai mahakamani hapo kuwa Julai 2,mwaka huu saa 11:00 jioni katika baa iliyo pia na nyumba ya kulala wageni iitwayo New M. Jokes iliyopo eneo la Maendeleo jijini Mbeya, chumba namba 11, mtuhumiwa Chelula alimdai rushwa ya ngono mwanafunzi huyo (jina linahifadhiwa), mwenye umri wa miaka 18.

Ilielezwa kuwa mtuhumiwa huyo alimdai mwanafunzi huyo wa kike anayesoma shule ya sekondari ya St.Aggrey ambayo yeye ni Mkuu wa shule, rushwa ya ngono kama sharti la kutoa huduma muhimu.

Chelula alikana shtaka hilo na yupo nje kwa dhamana hadi Julai 17,mwaka huu kesi hiyo itakapotajwa tena mahakamani hapo.

Wakati huo huo Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Mbeya, Respick Ndowo, alisema kuwa taasisi hiyo inaendelea na uchunguzi kuhusiana na rushwa ya ngono kwa mujibu wa kifungu cha sheria namba 25 cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa namba 11 ya mwaka 2007.

Ndowo alisema mtuhumiwa Chelula amefikishwa mahakamani ya mkoa Mbeya na ofisi ya mwanasheria wa serikali akikabiriwa na kosa la hilo la kubaka ambalo ni kesi ya jinai iliyopewa namba 135 ya mwaka huu.

JWTZ WAFANYA USAFI KATIKA MASOKO JIJINI MBEYA

WAFANYABIASHARA wa masoko ya Matola na Uhindini, yaliyopo jijini Mbeya, wamelipongeza Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), kwa kufanya usafi mkubwa katika masoko hayo jana.

Walisema kuwa hatua hiyo imezidi kuonyesha jinsi JWTZ linavyothamini na kuisaidia jamii katika mambo mengine ya kijamii mbali ya ulinzi wa mipaka ya nchi yetu.

Akizungumza na Uhuru kwa niaba ya wenzake, Makamu Mwenyekiti wa soko la Matola, Abdallah Shaibu, alisema wanalishukuru jeshi kwa uamuzi wa kwenda kuwafanyia usafi katika soko lao.

“Hii ni changamoto kubwa sana kwetu wafanyabiashara sokoni hapa tuliyopewa na JWTZ ya kuzingatia usafi wa soko hili kwa afya zetu na wananchi wanaokuja kununua mahitaji mbalimbali sokoni hapa” alisema Shaibu.

Aliongeza kuwa hali hiyo itasababisha wafanyabiashara hao waone kuwa usafi wa maeneo yanayolizunguka soko hilo ni muhimu na siyo kusubiria hadi wageni kutoka nje (JWTZ), ndio waende kuwafanyia kazi hiyo.

Shaibu aliwashauri wafanyabiashara wa masoko hayo ya Uhindini na Matola kuiga mfano huo wa kuzingatia usafi na kuyatunza maeneo yao kama walivyoonyeshwa na JWTZ na siyo kubweteka na kujua kazi ya usafi katika masoko hayo haiwahusu wao bali wafanyakazi wa halmashauri ya jiji la Mbeya.

Shaibu alisema:”Tunalishukuru sana JWTZ kwa uamuzi huu wa busara waliouchukua wa kuzijali afya zetu…walifika hapa saa 1:30 asubuhi na baada ya kufanya usafi soko lote waliondoka saa 3:30 asubuhi”.

DAWA ZA KUONGEZA MATITI,HIPS NA MAKALIO ZAKAMATWA IRINGA

MKAGUZI wa Dawa wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), kanda ya nyanda za juu kusini, Paul Sonda, amesema kuwa wamefanya ukaguzi wa ghafla na kulibaini duka moja mkoani Iringa, linalouza dawa za kuongeza matiti, makalio na Hips kwa wanawake.

Imeelezwa kuwa TFDA iliamua kufanya ukaguzi huo wa kawaida baada ya kupewa taarifa na raia wema kuwa duka hilo linauza dawa hizo ambazo zimetengezwa nchini China.

Akizungumza jana Sonda alisema kuwa baada ya kufanya ukaguzi huo walibaini kwamba dawa zote zinazouzwa dukani humo pamoja na jengo lenyewe vyote havijasajiliwa na TFDA.

“Tuliwahoji wauzaji ili kutaka kujua sehemu walikozinunua dawa hizo ambazo zimeandikwa kwa lugha ya Kichina lakini hawakuweza kuweleza kwani hata nyaraka walizonunulia hawakuwa nazo” alisema Sonda.

Alisema TFDA huwa wanasajili dawa zenye maandishi ya Kiingereza, Kiswahili ama zilizoandikwa kwa lugha zote hizo mbili lakini siyo nje ya hapo.

Mkaguzi huyo wa dawa kanda hii aliongeza kuwa dawa inaweza iikawa imeandikwa kwa lugha yoyote ile duniani lakini sharti ni kuwa lazima kuwepo na tafsiri ya maandishi hayo kwa Kiingereza ama Kiswahili.

Sonda alisema kuwa walitoa elimu kwa wauzaji wa duka hilo kuhusu umuhimu wa kusajili jengo hilo pamoja na bidhaa wanazouza ambapo walitoa ushirikiano mzuri.

Alisema:”Baadaye tulizichukua dawa hizo za kuongeza matiti, makalio na Hips na kuondoka nazo kwa kujibu wa taratibu zilizopo na tulikwenda kumkabidhi Mganga Mkuu wa hospitali ya mkoa wa Iringa kwa ajili ya kuziteketeza”.

Aliongeza kuwa hawakuweza kujua thamani halisi ya dawa hizo lakini zilikuwa nyingi na kuwa kwa ukaguzi walioufanya katika mikoa mingine ya Mbeya, Rukwa na Ruvuma hawajaweza kuzibaini dawa za aina hiyo.

Tuesday, July 7, 2009

MWANAFUNZI WA SEKONDARI YA IYUNGA MBEYA AGONGWA NA KUFARIKI

MWANAFUNZI wa kidato cha nne,shule ya sekondari Iyunga,jijini Mbeya amekufa papo hapo baada ya kugongwa na gari eneo la Nzovwe, akiwa anatembea pembezoni mwa barabara.

Ajali hiyo iliyohusisha gari ambayo ni daladala yenye namba za usajili T.129 AMD aina ya Toyota Hiace,ikiendeshwa na dereva Japhet Mwile, ilitokea jana saa 2:00 asubuhi katika barabara ya Mbeya kwenda Tunduma.

Kamanda wa polisi mkoa wa Mbeya,Advocate Nyombi, akizungumza jana ofisini kwake, alimtaja mwanafunzi huyo kuwa ni Hery Mlengule.

Nyombi alisema kuwa daladala hiyo ikiwa na abiria ndani yake ilikuwa inaelekea mji mdogo wa Mbalizi na mara baada ya ajalib hiyo, dereva pamoja na gari walipelekwa kituo kikuu cha polisi.

Uchunguzi zaidi juu ya ajali hiyo unaendelea kufanywa ili kujua chanzo cha ajali hiyo.

Katika tukio lingine lililotokea eneo la Forest Mpya, jijini hapa,mtoto mchanga wa kike mwenye umri kati ya wiki moja ama mbili aliokotwa akiwa ametupwa katika mfereji wa maji machafu na mtu asiyefahamika.

Kwa mujibu wa Kamanda Nyombi, tukio hilo lilitokea jana saa 11:00 jioni katika mtaa wa Kilimani uliopo eneo hilo.

Alisema kuwa mtoto huyo aliokotwa akiwa hai na Esther Mwakalebele, ambaye alikuwa anamwagilia bustani yake ya mboga mboga iliyopo jirani na mtaro huo wa maji machafu.

Nyombi alisema kichanga huyo yupo hai na anahifadhiwa hospitali ya Rufani Mbeya, kitengo cha Wazazi Meta na msako wa kumsaka mwanamke aliyefanya kitendo hicho cha kikatili unaendelea kufanywa.

SAMAKI WAPUNGUA ZIWA RUKWA-MBOZI

UVUVI haramu unaondelea kufanyika katika Ziwa Rukwa,upande wa wilaya Mbozi, umepelekea kupunguza kiwango cha uvuvi ziwani humo,imeelezwa.

Mkurugenzi Mtendaji wa wilaya ya Mbozi,Levisson Chilewa, alisema hilo limebainika baada ya kuona samaki wengi wanaovuliwa kutoka ziwani humo ni wale wadogo (wachanga).

Chilewa alisema kufuatia hali hiyo walitoa ombi kwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi, ili wafunge shughuli za uvuvi kwa miezi minne yaani kuanzia mwezi Januari hadi Aprili mwaka huu ili samaki waweze kuzaliana.

“Tuliona kuwa kipindi hiki ndio ambacho samaki huwa wanazaliana na kukua, hivyo tungeweza kutatua tatizo hili la upungufu wa samaki katika Ziwa hili upande wa Mbozi” alisema Chilewa.

Aliongeza kuwa njia nyingine wanayoitumia katika kukabiriana na hatari ya samaki kutoweka kabisa Ziwani humo, ni kujenga mabwawa 104 ya kufugia samaki ambapo katika viwanja vya ofisi ya halmashauri hiyo wanalo bwawa moja.

Mkurugenzi alisema kuwa bwawa hilo la halmashauri huwa linatumika kwa ajili kuzalisha samaki aina ya Perege ambao huwauza kwa wananchi, taasisi za kiserikali na zile zisizokuwa za kiserikali.

“Nia yetu ni kuhakikisha kuwa wananchi wananchi wanaendelea kutumia Samaki ili kuongeza lishe pia kujioongezea kipato zaidi” alisema Chilewa.

Aliongeza kuwa halmashauri imetengeneza boti ya kufanyia doria yenye thamani shilingi milioni 4.8 huku injini yake ikiwa na thamani ya shilingi milioni 2.8 kwa ajili ya kukabiriana na wavuvi haramu katika Ziwa hilo.

Chilewa alisema kwa kutumia boti hilo wameweza kukamata makokoro 37 na nyavu 110 zenye macho madogo ambazo hutumiwa na wavuvi haramu ambao wamepelekea kupungua kwa samaki Ziwani humo.

Ziwa Rukwa limepitia katika wilaya za Chunya na Mbozi kwa upande wa mkoa wa Mbeya na wilaya za Mpanda pamoja na Sumbawanga Vijijini,kwa mkoa wa Rukwa.