Monday, July 27, 2009

SUMATRA KUDHITI DALADALA ZISIZTIKETI KWA ABIRIA JIJINI MBEYA.

MAMLAKA ya Udhibiti Wa Usafiri Nchi kavu na Majini (SUMATRA), kanda ya nyanda za juu kusini, imeazimia kupambana na tatizo sugu la wamiliki wa daladala jijini Mbeya la kutopenda kutoa tiketi kwa abiria.

Imeelezwa kuwa tatizo la utoaji wa tiketi kwa abiria wa daladala jijini Mbeya, limekuwa sugu hali inayopelekea abiria wengi wanaotumia usafiri huo kuona kama ni kawaida kwa wao kutopatiwa tiketi.

Akizungumza ofisini kwake, Ofisa Mfawidhi wa SUMATARA kanda, Amani Shamaje, alisema kuwa wamedhamiria kukomesha tabia hiyo ambayo imekuwa kero kwa abiria wengi.

Shamaje alisema kuwa tatizo hilo lilikuwepo pia kwa mabasi yafanyayo safari kwenda wilayani, lakini hivi sasa limekwisha baada ya SUMATRA kuingilia kati na kuanza kuyakamata mabasi hayo na kutoza faini ya shilingi 250,000 kwa kila basi lililokuwa halitoi tiketi kwa abiria.

"Hivi sasa mabasi mengi yafanyayo safari za kwenda wilayani yamekuwa yanatoa tiketi kwa abiria...tatizo tulilonalo sasa ni utoaji wa tiketi kwa daladala zifanyazo safari hapa jijini Mbeya" alisema Shamaje.

Aliongeza kuwa waliamua kwanza kutilia mkazo suala la uvaaji wa sare kwa madereva na makondakta wa daladala na pia kupiga marufuku usimamaji kwa sehemu zisizo kuwa na vituo ambapo wameweza kufanikiwa kwa kiwango kikubwa.

Ofisa Mfawidhi huyo wa SUMATRA kanda ya nyanda za juu kusini, alisema utoaji wa tiketi kwa abiria wa daladala jijini Mbeya, limekuwa ni tatizo linalowasumbua kwa muda mrefu na wameamua kujipanga ili kuhakikisha kuwa wanalimaliza.

Alisema kuanzia sasa daladala yoyote inayofanya safari zake jijini Mbeya, ambayo itakuwa haitoi tiketi kwa abiria itakuwa inatozwa faini ya shilingi 250,000 au kifungo cha kuanzia mwaka mmoja ama kisichopungua miwili au adhabu zote kwa mpigo.

Katika hatua nyingine, Shamaje alisema kuwa wanaandaa mkakati wa kuwadhibiti madereva wa daladala zinazotoka jijini Mbeya kwenda mji mdogo wa Mbalizi, ambazo zimekuwa hazifiki mwisho wa safari na badala yake kuishia eneo la Iyunga na hivyo kupelekea usumbufu kwa abiria.

Alisema kuwa watakutana na Mkuu wa kikosi cha Usalama barabarani mkoa wa Mbeya, Ezekiel Mgeni, ili kuangalia njia sahihi za kukomesha tabia hiyo ambayo hufanywa kuanzia saa 12:00 jioni ambayo imekuwa inapelekea abiria walazimike kupanda mabasi mawili tofauti ili kukamilisha safari

."Huu ni usumbufu kwa abiria kwani unakuta gari limeandikwa kuwa linakwenda Mbalizi, lakini likifika Iyunga abiria wanaambiwa kuwa hapo ndio mwisho wa safari...hii ni usumbufu kwani huwalazimu abiria kupanda daladala lingine ili kuwawezesha kukamilisha safari" alisema Shemaje.

No comments:

Post a Comment