UONGOZI wa hospitali ya Rufaa Mbeya, umetakiwa kuwalipa wafanyakazi wake malipo ya saa za ziada kwa kufuata ngazi za mshahara (TGHS), na siyo utaratibu uliopo sasa.
Imeelezwa kuwa uongozi huo umekuwa ukiwaweka maofisa katika makundi mawili, lakini wote wamekuwa wakilipwa saa za ziada kwa kima cha chini cha mshahara, hali ambayo inakuwa haiwatendei haki.
Hayo yalisemwa jana na Mwenyekiti wa Chama Cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE), hospitalini hapo, Ismail Zambi, wakati wa hafla ya kuwapa zawadi wafanyakazi bora wa Sikukuu ya Wafanyakazi duniani(Mei Mosi), mwaka huu, iliyofanyika hospitalini hapo.
Mgeni rasmi katika tukio hilo, alikuwa Rais wa Shirikisho la Vyama Vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Ayuob Omary.
Wafanyakazi saba walipewa zawadi zao akiwemo mfanyakazi bora wa hospitali hiyo kwa mwaka huu ambaye ni muuguzi mkunga, Regina Sithole, aliyezawadiwa shilingi 300,000.
Zambi alisema utaratibu huo unaofanywa na hospitali ya Rufaa Mbeya siyo sahihi kwani umekuwa unawatambua maofisa wenye elimu ya digrii kitu ambacho siyo sahihi.
"Tumekuwa tunawekwa matabaka mawili tofauti wakati kazi ni zile zile...hivyo ingekuwa vyema wangeweka utaratibu wa kuangalia TGHS kwani Utumishi unatutambua kuwa ni maofisa wakati uongozi wa hospitali unamtambua ofisa kuwa ni yule mwenye digrii" alisema Zambi.
Aliongeza kuwa pia kuna mapungufu mengine yaliyopo hospitalini hapo ikiwemo kutowapandisha vyeo wafanyakazi kwa wakati kwa mujibu wa taratibu zilizopo.
Mwenyekiti huyo wa TUGHE alisema vile vile kumekuwepo na tatizo la kutorekebishwa mishahara kwa wakati kwa wanaopandishwa vyeo, kutolipwa mapunjo ya mishahara kwa wanaopandishwa vyeo na kurekebishiwa mishahara yao.
Zambi alisema:"Tunaupongeza uongozi wa hospitali kwa kudumisha utaratibu huu wa kutoa zawadi kwa watumishi hodari wakati wa sherehe za Mei Mosi kwa kila mwaka...".
Naye Rais wa TUCTA Omary alipongeza hatua hiyo ya kuwapatia zawadi watumishi bora, lakini pia alikumbushia kuhusu umuhimu wa kufanya vikao mahali pa kazi kwa kufuata utaratibu uliopo.
Omary alisema kuwa kwa kupitia vikao hivyo uongozi na wafanyakazi wanaweza kuvitumia kuweka wazi kasoro mbalimbali zinazokuwepo na hivyo kuweza kuzipatia ufumbuzi wake.
"Kwa kuwapa zawadi watumishi wenu bora mnakuwa mnawajengea motisha zaidi ya kuwajibika zaidi" alisema Omary.
Wafanyakazi wengine waliopata zawadi zao za shilingi 150, 0000 kila mmoja ni Dk.Henry Mwakayoka, ofisa wa maabara Hilary Mchuka, ofisa muuguzi kitengo cha wajawazito na Watoto Meta, Mwanjaa Kasigwa na ofisa muuguzi kitengo cha huduma ya afya ya akili, Daina Ifwani.
Pia wamo Muuguzi mkunga wa kitengo cha kuhudumia wanaoishi na virusi vya Ukimwi, Eddah Sanjala na Ally Mbasha kutoka upande wa masijala katika sehemu ya utawala.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment